Social Icons

Loading...

SAFARI YA STARS FAINALI ZA CHAN YAISHIA UGANDA

Ndoto ya Timu ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars kushiriki fainali za Afrika kwa wachezaji wa Ligi za Ndani (CHAN) ‘zilipeperuka’ jana kwa kipigo cha mabao 3-1 kutoka Timu ya Taifa ya Uganda, The Cranes katika mchezo wa marudiano kwenye Uwanja wa Namboole, Kampala.
Safari ya Stars imepotea kwenye michuano hiyo itakayopigwa Afrika Kusini mwakani, baada ya kufungwa nyumbani na ugenini na kufanya matokeo ya jumla kuwa mabao 4-1.
Taifa Stars, ambayo ilishiriki fainali za kwanza za CHAN kule Senegal mwaka 2009 chini ya Kocha Mbrazil, Marcio Maximo, sasa itasubiri kucheza tena michuano hiyo mwaka 2016.Matokeo hayo yanaifanya Uganda kuendelea kuifunga Tanzania inavyotaka, kwani katika mechi 41 walizokutana, wameshinda mechi 25 dhidi ya mechi 11.
Katika mchezo huo, wenyeji Uganda wakicheza kwa kujiamini, walikuwa wa kwanza kulifikia lango la Tanzania katika dakika ya kwanza na sita baadaye waliandika bao la kwanza.
The Cranes walifunga bao hilo wakitumia makosa ya mabeki wa Stars walioshindwa kujipanga vizuri na kumruhusu Mpande Joseph kuruka juu bila kukabwa na kupiga kichwa mpira uliomkuta Kalanda Frank aliyemtungua kipa Juma Kaseja.
Uganda walirudi kwenye uongozi mwanzoni mwa kipindi cha pili kwa kufunga bao la pili lililotokana na kiki ya penalti ya Brian Majwegwa kutokana na beki wa Stars David Luhende kuucheza mpira kwa mkono alipokuwa kwenye harakati za kuondoa hatari.
Safari ya Taifa Stars kwenda Afrika Kusini ilizidi kupotea baada ya wenyeji Uganda kufunga bao la tatu kutokana na shambulizi la kushtukiza katika dakika ya 47.
Hakuna shaka, bao hilo lililofungwa na Frank Kalanda lilitokana na uzembe wa kiungo Abubakary Salum, ambaye jaribio lake la kutaka kuumiliki mpira mbele ya wachezaji wawili wa Uganda lilishindikana na hivyo kuwapa mwanya wa kufanya shambulizi la kushtukiza.
Bao pekee la Stars lilifungwa dakika ya 17 na Amri Kiemba kwa shuti la nje ya 18 akimalizia kazi nzuri ya winga Mrisho Ngasa aliyecheza vizuri kipindi cha kwanza.
Mbali na mabao hayo, Stars wangeweza kuwa mbele kwa mabao 2-1 katika dakika ya 35, kama siyo kiki kali ya umbali mrefu iliyopigwa na Ngasa na kugonga ‘paa’ la Uganda na mpira kurudi uwanjani.
Kipa na nahodha wa Stars, Kaseja alifanya kazi ya ziada kupangua shuti kali la Mpande Joseph, huku dakika ya 11 mpira wa kichwa kutoka wa beki Aggrey Morris ukipaa juu kidogo ya lango kufuatia kona ya Erasto Nyoni.
author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

CodeNirvana
© Copyright Daniel Blog in Contemporary News
Back To Top