Social Icons

Loading...

NMG yapata ofisa mtendaji mkuu mpya

Mr   Joseph   Muganda
Bodi ya Wakurugenzi ya Kampuni ya Nation Media Group (NMG) imemtangaza Joseph Muganda kuwa Mkurugenzi Mtendaji na Ofisa Mtendaji Mkuu mpya atakayeshika hatamu ya uongozi wa kampuni hiyo kuanzia Julai Mosi mwaka huu.
NMG inamiliki vyombo vya habari Kenya, Tanzania, Uganda na Rwanda.
Uteuzi wa Muganda umekuja baada ya Mkurugenzi Mtendaji na Ofisa Mtendaji Mkuu aliyepo, Linus Gitahi kuomba kustaafu mapema ili aendelee na shughuli zake binafsi.
Taarifa iliyotolewa na NMG ilieleza kuwa Muganda ni mtendaji mwandamizi mwenye uzoefu mkubwa katika tasnia ya utawala na masoko na amejiunga na kampuni hiyo ya habari Afrika Mashariki na Kati akitokea Kampuni ya Bia ya Kenya (KBL) akiwa pia ni Mkurugenzi Mtendaji.
Akitangaza mabadiliko hayo jana, Mwenyekiti wa Bodi ya NMG, Wilfred Kiboro alitoa shukrani kwa Gitahi kwa mchango wake katika maendeleo ya kampuni kwa kipindi cha miaka minane aliyotumikia katika cheo hicho.
Alisema Gitahi alisimamia uanzishwaji wa bidhaa na huduma mpya na upanuzi wa kampuni katika masoko mapya na kuongeza mauzo kutoka Sh116.5 bilioni hadi Sh247.9 bilioni. Pia, aliongeza faida ya kampuni kabla ya kodi kutoka Sh22.2 bilioni hadi Sh66.6 bilioni.
Kiboro alimweleza Gitahi kuwa alikuwa mfano wa kuigwa kiuongozi katika kipindi kigumu katika uendeshaji wa sekta ya habari nchini Kenya na Afrika Mashariki kwa ujumla.
Gitahi ataendelea kusimamia shughuli za NMG hadi Juni 30 mwaka huu kabla ya kukabidhi ofisi kwa Muganda na pia atatoa huduma za ushauri hadi mwishoni mwa mwaka.
Akimkaribisha Muganda katika kampuni ya NMG inayomiliki pia kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL) inayochapisha magazeti ya Mwananchi, The Citizen na Mwanaspoti, Kiboro alisema:
“NMG inayo furaha kumkaribisha Muganda katika timu yetu ambapo analeta utaalamu wa masuala ya masoko, usimamizi wa mawasiliano, mashirika na udhibiti na utendaji ambao umejengwa na uzoefu wa kipindi kirefu katika mashirika mbalimbali ya kimataifa barani Afrika.”
Kwa upande wake, Muganda alisema anayo furaha kujiunga na NMG na kujumuika katika utekelezaji wa kazi na wajibu wa kuwa chombo cha habari chenye ubora wa hali ya juu na huru katika kukuza maendeleo ya jamii.
author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

CodeNirvana
© Copyright Daniel Blog in Contemporary News
Back To Top