Rais Jakaya Kikwete ameongoza maelfu ya waombolezaji kumzika
aliyekuwa Askofu Mkuu Moses Kulola wa Kanisa la Evangelist Assemblies of
God Tanzania (EAGT). Kiongozi huyo alizikwa jana nje ya Kanisa la
Calvary Bugando.Licha ya kuongoza mazishi hayo, Rais Kikwete pia
alitoa ushuhuda kwamba licha ya kuwa muumini wa dini ya Kiislamu, Askofu
Kulola wakati wa uhai wake mara kadhaa alikwenda Ikulu kumfanyia
maombi.
Rais Kikwete katika salamu zake za rambirambi,
alisema amekwenda kushiriki msiba huo kuungana na waombolezaji kutokana
na kumfahamu Askofu Kulola ambaye alikuwa mtu wa watu.
“Tuzidi kuwaombea kwa Mungu, familia katika
kipindi hiki kigumu, kwa jinsi nilivyomfahamu marehemu alikuwa mpenda
watu, hakujali kabila wala hali zao, alijali utu na heshima hii ndiyo
sababu na mimi alikuwa rafiki yangu,” alieleza Rais Kikwete.
Alibainisha kwamba licha ya kuwa Muislamu mara
kadhaa Askofu huyo alifika kumwombea Ikulu na katika maombezi yake
alisisitiza kuwa alikuwa akiwaombea Watanzania na nchi nzima kwa ujumla,
hivyo aliwahimiza walio hai kumuenzi Askofu kwa vitendo.
Post a Comment