Social Icons

Loading...

RAI YA JENERALI : Hii ni harufu mbaya tu, Ibilisi bado hajaenda msalani

 BAADHI ya masuala ambayo nimekuwa nikiyajadili yanajitokeza hivi sasa kwa mshindo mkuu.Nimekuwa nikisema kwamba tunajitahidi mno kujenga taifa dogo ndani ya nchi kubwa. Hili linadhihirika sasa. Nimekuwa nikisema pia kwamba tunaonekana kuwa na haraka ya kufanya mambo kama vile tunakwenda kwingine, hapa si kwetu na wala hatujafika. Hili nalo linajionyesha.
    Hivi sasa tumetekwa na kelele zinazopigwa kuhusu gesi asilia inayochimbwa kusini mwa Tanzania, na tayari tumeanza kuona dalili za nchi kuparaganyika kutokana na ‘utajiri’ huo.Tunachokishuhudia si mjadala wa jinsi gani tunaweza kunufaika kama taifa kutokana na gesi inayochimbwa nchini ( na pia utajiri mwingine unaotokana na rasilimali za nchi) bali ni ghadhabu za makundi hasimu yanayokinzana kuhusu namna ya kugawana kidogo tulicho nacho.

    Kwa muda sasa, wataalamu duniani wamekuwa wakijadili kile kinachoitwa ‘resource curse’, au laana ya rasilimali. Hii ni laana ya nchi kama yetu ambazo zinajikuta zikiwa na rasilimali kubwa, lakini badala ya rasilimali hizo kuzinufaisha nchi hizo inageuka kuwa ni balaa, laaana. Hili ndilo linaelekea kutokea hapa nchini.Bado hatujui kwa uhakika ni kiasi gani cha gesi asilia tulicho nacho. Nimesoma mahali kadhaa kwamba gesi hii ni nyingi mno na inaweza ikaifanya Tanzania kuwa mojawapo ya nchi zenye machimbo ya gesi makubwa duniani. Bila shaka hilo lingekuwa jambo jema kwa nchi inayoendeshwa kwa utaratibu unaoeleweka na inayojadili masuala muhimu kwa uwazi wa kutosha.
    Kwa bahati mbaya, hii si kweli. Tumekuwa tukishuhudia usiri unaogubika mikataba juu ya rasilimali nyingine kwa muda mrefu sasa, na hakuna dalili kwamba tutaanza kesho au keshokutwa kuwa wawazi zaidi.Hadi leo serikali inakataa kuanika hadharani maudhui ya mikataba inayoingia kwa niaba ya Watanzania, na serikali  ikiulizwa inajibu kwamba mikataba hiyo ni siri baina ya serikali na ‘ wawekezaji.’
author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

CodeNirvana
© Copyright Daniel Blog in Contemporary News
Back To Top