Social Icons

Loading...

Utata Wagubika ARV Bandia

UTATA umegubika kuwapo kwa dawa bandia za kupunguza makali ya virusi vya Ukimwi (ARV), baada ya ripoti ya Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) kutofautiana na maelezo ya wizara, kuhusu kiasi kilichosambazwa na madhara yake katika jamii.
Wakati Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii ikisema haijajua kiasi halisi cha dawa hizo, lakini ikisisitiza kwamba athari zake ni kidogo, TFDA imeeleza kuwa makopo 1,360 yalibainika katika utafiti wake mkoani Mara kuwa yako mikononi mwa wagonjwa.

Kwa mujibu wa taarifa ya wizara hiyo iliyotolewa na Kaimu Katibu Mkuu, Regina Kikula Ijumaa, hadi kufikia Septemba 4, mwaka huu makopo 8,008 ya toleo namba OC.01.85 ya dawa hizo yalikuwa yamezuiwa. 
Taarifa ya TFDA
Taarifa ya jopo la wataalamu wa TFDA waliofanya ukaguzi katika baadhi ya hospitali na vituo vya afya mkoani Mara, inaonyesha kuwa zaidi ya makopo 1,360 yalishatolewa kwa wagonjwa.

Mtaalamu mmoja wa dawa aliliambia Mwananchi kuwa katika makopo hayo baadhi huwa na vidonge 30 na mengine 60.“Kopo lenye vidonge 60 hutumiwa na wagonjwa ambao humeza dawa hizo mara mbili kwa siku, asubuhi kimoja na jioni kimoja, lenye vidonge 30 hutumiwa na wagonjwa wanaomeza kidonge kimoja tu kwa siku,” alisema daktari huyo.

Ukaguzi wa TFDA, katika Hospitali ya Mkoa wa Mara ulibaini kwamba, dawa aina ya TT-VR30 zilizokuwapo katika hospitali hiyo zilikuwa zimeingizwa kutoka nje ya nchi.

Ulibaini pia kuwa, wagonjwa wamekuwa wakitumia dawa hiyo peke yake (monotherapy) kwa muda mrefu badala ya kuchanganywa na nyingine, hivyo kuwapo kwa uwezekano mkubwa wa virusi ya Ukimwi kujenga usugu. “Tulipokagua, tulibaini kuwapo kwa batch (toleo) tatu za dawa hiyo ambazo ni OB.15.85, OB.18.85 na OC.01.85, ambapo batch mbili za kwanza zote hazikuwa na matatizo, isipokuwa batch namba OC.01.85 ambayo ilikuwa na matatizo,” inaeleza sehemu ya ripoti hiyo ya TFDA.

Inaeleza kwamba, katika hati ya malipo ya kupelekwa kwa dawa hizo kutoka MSD, matoleo mawili ya kwanza yaani OB.15.85 na OB.18.85 pekee ndizo zilizoandikwa, toleo namba OC.O1.85 haikuandikwa, ingawa msimamizi wa bohari ya hospitali hiyo, aliwaeleza wataalamu wa TFDA kuwa dawa hizo zilifikishwa hapo Mei, mwaka huu.

“Katika kukagua dawa zilizokuwa ndani ya makopo hayo, tulibaini baadhi ya makopo yalikuwa na vidonge vyenye rangi mbili tofauti, wakati makopo mengine yalikuwa na vidonge vya njano kama aina ya Efavirenz,” inasema ripoti hiyo.Inafafanua kuwa, baadaye wataalamu hao waligundua kuwa vidonge vyenye rangi mbili ni aina ya NEVILAST-30, vilivyotengenezwa na Kiwanda cha Hetero Drugs cha India.

Inabainisha kwamba vidonge vya njano ni aina ya Efavirenz vilivyotengenezwa pia na Kiwanda cha Hetero Drugs, India, vyote vikiwa vimehifadhiwa katika makopo yenye alama ya TT-VR30.“Tulipolinganisha makopo ya dawa hizo, tulibaini kuwa makopo yaliyokuwa na vidonge vyenye rangi mbili, (NEVILAST-30) vidonge vyake vilikuwa katika kopo pana na lenye mfuniko mpana,” inaeleza ripoti hiyo na kuongeza:

“Vidonge vyenye rangi ya njano (efavirenz) vilihifadhiwa katika kopo dogo, jembamba na lenye mfuniko mdogo.”Kwa mujibu wa ripoti hiyo wataalamu hao walifanya ulinganisho huo kirahisi baada ya kufanya ukaguzi katika Kituo cha Afya Nyasho, kilichopo Musoma, ambacho hutumiwa kama kituo kikuu cha Manispaa kwa kusambazia dawa za kupunguza makali ya Ukimwi.

“Katika kituo hicho hakukuwa na dawa aina ya TT-VIR30, isipokuwa NEVILAST-30 na Efavirenz. Kulikuwa na mazingira yaliyoonyesha kuwa dawa hizo zilitoka MSD kama baadhi ya boksi za dawa zilivyoandikwa, kuonyesha kuwa dawa hizo zilikuwa zinakwenda MSD Mwanza na baadaye mkoani Mara,” inaeleza.Inabainisha kuwa, jumla ya dawa zilizobainika kuwa na matatizo hayo na ambazo zilizuiliwa kutumika katika hospitali hiyo zilikuwa katika makopo 216, wakati makopo 800 tayari dawa zake zilishagawiwa kwa wagonjwa.

“Baada ya ukaguzi, tuliandika taarifa ya yale tuliyoyabaini, kuchukua sampuli na kivuli cha invoice (hati ya malipo) ya MSD kilichukuliwa. … Tulielekea wilayani Tarime na kufanya ukaguzi katika Hospitali ya Wilaya,”  sehemu ya taarifa hiyo inaeleza.Inaweka wazi kuwa katika ukaguzi huo walibaini kuwapo kwa dawa aina ya TT-VIR30 inayotengenezwa na Kiwanda cha TPI cha mjini Arusha.

Wataalamu hao pia walibaini kuwapo kwa toleo la nne la dawa aina ya TT-VIR30, la kwanza likiwa namba OB.03.85, la pili OB.06.85, la tatu 0B.18.85 na nne OC.01.85, ambalo lilibainika kuwa na matatizo. Wataalamu hao walipochunguza vidonge vilivyokuwa ndani ya makopo hayo walibaini kuwa vidonge vyote vilikuwa vyenye rangi mbili pekee na hakukuwa na vidonge aina ya efavirenz vilivyoonekana katika makopo hayo. Ripoti hiyo inaweka wazi kuwa, vidonge vingi kati ya hivyo vilikuwa vimeharibika na kuota ukungu na kwamba makopo yote yaliyokuwa yametumika yalikuwa ya dawa aina ya NEVILAST-30.

Inasema kuwa, taarifa ya hospitali hiyo inaonyesha kuwa dawa hizo zilifika hapo kutoka MSD, Mei 8, mwaka huu. "Katika invoice ya MSD batch moja tu yaani OB.15.85 ndiyo iliyoandikwa. Batch nyingine tatu haikujulikana kwa nini hazikuandikwa,” ripoti hiyo inaeleza.

Inafafanua kuwa, makopo yaliyobainika kuwa na matatizo katika Hospitali ya Wilaya ya Tarime ni 86 na haijulikani ni mangapi yaliyotolewa kwa wagonjwa.Ili kujiridhisha na kuwapo kwa dawa hiyo katika wilaya nyingine, ripoti hiyo inaeleza kwamba wataalamu hao walifanya mawasiliano na mtunza stoo wa Hospitali Teule ya Nyerere wilayani Serengeti na kwamba taarifa walizopewa zilionyesha kuwapo kwa dawa aina ya TT-VR30 katika hospitali hiyo.

Kuhusu dawa toleo namba OC.01.85 katika hospitali hiyo ilielezwa kuwa na matatizo na kwamba msimamizi huyo alipofungua kopo moja moja, alibaini makopo yote yalikuwa na vidonge aina ya NEVILAST-30 vyenye rangi mbili.Mtunza stoo huyo aliwaambia wataalamu wa TFDA kuwa dawa hizo zilipelekwa hospitalini hapo Mei 8, mwaka huu.

Kwa mujibu wa TFDA katika hospitali hiyo ya Nyerere, kulikuwa na makopo 288 ya dawa hizo na kwamba katika Wilaya ya Rorya, Hospitali ya Shirati pia kulikuwa na dawa hizo zilizopokewa kutoka Hospitali Teule ya Wilaya ya Bunda.

“Mei walipokea makopo 596 na kati yake yamebaki 36 tu, walieleza kuwa hawakuwa na invoice ya MSD kwa kuwa dawa hizo hawakupelekewa na MSD moja kwa moja, bali walizipata kutoka Bunda,” inasema ripoti ya TFDA ikiongeza: “Jambo la kusikitisha ni kuwa, baadhi ya makopo yana aina ya Efavirenz ambazo hupaswa kutumiwa mara moja, tena nyakati za usiku tu. Hivyo wagonjwa waliotumia dawa hizo wamekuwa wakitumia dawa moja (monotherapy) kwa muda mrefu na hivyo kuna uwezekano mkubwa wa virusi kujenga usugu.” Inasema kuwa, katika ukaguzi waliofanya mkoani Mara, wataalamu hao walibaini kuwapo kwa dawa hizo bandia kwa kiwango kikubwa.“Vilevile kuna taarifa zinazoonyesha kuwa dawa hizo zilitoka MSD Makao Makuu (Dar es Salaam) na Ofisi ya Kanda ya Ziwa,” inasema taarifa hiyo.

Wataalamu hao katika taarifa yao hiyo, walishauri ukaguzi ufanyike katika kanda nyingine na kwamba lengo liwe kuangalia hospitali na vituo vya afya vilivyogawiwa dawa za ARVs mwezi Mei.

Kauli ya Wizara
Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imeeleza kuwa haijapata kiwango halisi cha dawa hizo bandia ambacho tayari kilikuwa kimeshasambazwa kwa watumiaji.Kaimu Katibu Mkuu wa wizara ya hiyo, Regina Kikula, alipoulizwa na Mwananchi kuhusu kiwango cha dawa hizo ambacho kilikuwa kimeshasambazwa, alisema kuwa bado wanafanya uchambuzi na kwamba hakuna taarifa rasmi.

Hata hivyo Kikula alisisitiza kwamba wizara bado inaendelea kulifuatilia suala hilo kwa karibu na kwamba baada ya kukamilisha uchunguzi itatoa taarifa kamili.“Baada ya kupata taarifa hizo, tuliwatuma watu wetu katika mikoa yote mitatu ambako taarifa za kuwapo kwa dawa hizo zilipatikana (Mara, Tanga na Dar es Salaam), na hicho ndicho kiwango tulichokipata, lakini bado kuna taarifa hatujazipata vizuri,” alisema Kikula na kuongeza:

"Naomba tupewe muda tuhitimishe uchunguzi wetu kisha tutatoa taarifa kamili, lakini nawahakikishia wananchi waendelee kutumia tu, hali ni salama kwa kuwa dawa hizo tayari zimeshazuiliwa na kuondolewa."Kuhusu wahusika wa dawa hizo alisisitiza kuwa baada ya kukamilika kwa uchunguzi, wale watakaobainika kuhusika kwa namna moja ama nyingine kuingiza dawa hizo sokoni, watachukuliwa hatua za kisheria.
Habari  kwa  hisani  http://www.mwananchi.co.tz/habari/-/26210-utata-wagubika-arv-bandia
author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

CodeNirvana
© Copyright Daniel Blog in Contemporary News
Back To Top