Wakati raia tisa wa China wakibainika kuugua ugonjwa wa dengue na kulazwa hapa nchini, Rais Jakaya Kikwete amevunja ukimya na kuagiza wizara zake mbili kukabiliana na ugonjwa huo kwa dharura.
Ugonjwa huo uliingia nchini tangu mwaka 2010 
lakini mlipuko wake mkubwa ulibainika Machi mwaka huu na hadi jana 
wagonjwa zaidi ya 400 walikuwa wameambukizwa, huku watatu wakiripotiwa 
kufariki dunia, akiwamo Daktari Bingwa wa magonjwa ya akili, Dk Gilbert 
Buberwa anayezikwa leo, Dar es Salaam.
                
              
Rais jana aliziagiza Wizara ya Afya na Ustawi wa 
Jamii na ile ya Fedha kushirikiana Bohari Kuu ya Dawa (MSD) kuchukua 
hatua za dharura kupambana nao kwa kuhakikisha vinapatikana vipimo vya 
kutosha na dawa.
                
              
Wachina walazwa
                
              
Taarifa kutoka Hospitali ya Aga Khan, Dar es 
Salaam zilieleza kuwa wagonjwa waliobainika kuugua homa hiyo hadi jana 
ni raia hao wa China na Watanzania wachache wenye historia ya kusafiri 
nje ya nchi hasa China, Ufilipino na Kusini mwa India.
                
              
Muuguzi katika kitengo cha magonjwa ya kuambukiza 
cha Aga Khan, Nyangee Lugoe alisema hospitali hiyo ilianza kupokea 
wagonjwa tangu Machi mwaka huu na kuanzia Aprili, raia wengi wa China 
wamegundulika kuwa na homa hiyo, ingawa baadhi walitibiwa na kuruhusiwa.
                
              
Agizo la Rais Kikwete
                
              
Akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Wauguzi 
Duniani huko Arusha, Rais Kikwete alisema: “Hili ni jambo la dharura la 
kitaifa lazima hatua muafaka zichukuliwe kudhibiti ugonjwa huu, ambao 
asili yake ni nchi za Asia na Bara la Amerika.”
                
              
Alisema dalili za ugonjwa huo ambao unasababishwa 
na mbu aina ya Aedes Egyptie anayeuma mchana ni homa kali ya kuumwa 
kichwa, maumivu ya viungo na kutoka damu puani na kwenye fizi na 
kupoteza fahamu.
                
              
“Napenda kutoa wito mtu yoyote ambaye atapata 
dalili za ugonjwa huu, aende mara moja hospitalini ili afanyiwe vipimo 
badala ya kunywa dawa,” alisema.
                
              
Tayari Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii 
imetangaza kuanza kuchukua hatua za dharura kukabiliana na ugonjwa huo, 
ikiwa ni pamoja na uelimishaji na uhamasishaji wa jamii kuchukua 
tahadhari.
                
              
Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Charles Pallangyo 
alisema jana kuwa wizara yake imetoa hadhari ya ugonjwa huo kupitia kwa 
waganga wakuu wa mikoa na wilaya kote nchini na itatoa mafunzo maalumu 
kwa watumishi wa afya ikiwajumuisha madaktari na mafundi maabara ili 
kuwajengea uwezo.






Post a Comment